Monday 3 December 2012

FREDY MTOY HATUNAE TENA- IBADA YA KUMUIGA YAONYESHA UMAHIRI WAKE KATIKA KAZI

“Alikua mfano dhahiri wa neno mtanashati”-Zawadi Machibya, mratibu wa msiba na mtangazaji wa BBC Swahili

Na: Freddy Macha

Kanisa la St Annes Lutheran katikati ya jiji la London juzi Jumamosi lilikuwa kituo maalum cha kumwaga na kuwa wasifu wa maisha  ya marehemu Freddy Alex Mtoi aliyekuwa mtangazaji wa BBC Swahili kwa miaka mingi.
 
Ibada hiyo iliyoendeshwa na wachungaji  Tumaini Kalaghe na Mathew Jutta, ilihudhuriwa na wanahabari mbalimbali kutoka BBC , Ofisa wa Ubalozi wa Tanzania, Clement Kiondo, marafiki wa karibu waliomjua marehemu na wanananchi wa sehemu toka Tanzania, Afrika na Ulaya. 

Mratibu wa mazishi , Zawadi Machibya, ambaye ni mtangazaji wa BBC,  aliendesha shughuli na kuwajulisha wasemaji wote waliozungumzia kwa kuanza kueleza namna neno “mtanashati” lilivyomvaa Freddy Mtoi aliyefariki usiku wa kuamkia Jumamosi tarehe 17 Novemba, 2012. 

Mchungaji Mathew Jutta alikumbusha kwamba safari yetu wanadamu huanzia kwa Mungu na kuishia kwa  Mungu. Akailinganisha nsafari hiyo na ile ya kutoka nyumbani Afrika kuja Majuu (ambapo paliitwa Mtoni enzi mchungaji alipokuja Ulaya takribani miaka 20 iliyopita). “Kwa wanaobakia ni huzuni lakini kwa anayesafiri ni furaha yenye matumaini.”  Akimzungumzia marehemu alitaka zaidi kututuliza roho tuliyobakia.
 
Maneno haya yalisimama dede kama dhamira kuu ya msiba. Kwamba badala ya kuhuzunika tujiratayarishe tunakokwenda kwa kuzingatia maneno ya Biblia, Yohana Mtakatifu 3:20 : “ Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa.”

Wafanyakazi wenzake marehemu Mtoi nao waliendeleza hoja kwa kutueleza  undani wa bidii yake marehemu kazini, tabia yake ya uungwana na upole. Akifafanua kwa kina, mtangazaji  wa BBC toka Kenya Solomon Mugera alitoa mfano namna marehemu alipokuwa tayari kumenyeka hata wakati wenzake wakitaka kupumzika kama wakati wa sikukuu ya Krismasi.  Mugera :“ Marehemu hakuwa mlalamishi au mbishi. Alikua haogopi kufanya kitu ambacho hakifahamu.”
Akitoa maelezo katika lugha ya Kiswahili na Kiingereza kwa niaba ya wageni wengine, Solomon alitaja mfano mwingine mkubwa wa  jinsi Mtoi alivyokua mchapa kazi asiyenung’unika kiasi ambacho hata alipokuwa mgonjwa aliwaambia wenzake “ni kitu kidogo tu” wasitie shaka, kumbe mwenzetu alikua akielekea katika kifo.

Salim Kikeke mtangazaji  gwiji  aliyefanya kazi na marehemu toka Bongo miaka kumi iiliyopita alitukumbusha zaidi kwa undani vipindi Freddy Mtoi alivyovitoa kwa kuacha sauti yake isikike kwa wastani wa dakika moja.
 
 Hapo tulimsikia akiwahoji wananchi mbalimbali mitaani Uingereza. Mfano  kipindi alichowauliza watu maana ya  mti wa Krismasi, unaothaminiwa sana na Wazungu. Kati ya wahojiwa alikuwa mchungaji  Tumaini Kallaghe aliyeongoza sala hii  juzi.
 
Tulipata vile vile fursa ya kusikiliza sauti za wazazi wake Mtoi wakieleza namna alivyokuwa mtoto mwenye bidii, mtiifu na aliyeanza kuipenda kazi ya uanahabari toka angali mdogo sana.  
 
Mbali na wafanyakazi walikuwepo pia marafiki zake wa karibu , mathalan Prochest Tairo aliyefuta dhana iliyoenea ( toka msiba ulipotokea) kwamba marehemu alikuwa msiri na mtu wa kujificha. 
 
Tairo ambaye pia ni bloga na alimjua Mtoi toka wakisoma wote sheria  chuo kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1997- 2002 alisema: “Kwa nje alikuwa akionekana mkimya sana, mkiongea anasikiliza anatabasamu. Lakini ukishamzoea ni mzungumzaji sana...si kweli alikuwa mkimya, ila ilibidi akuzoee.”
 
Aliongeza kueleza marehemu alipenda mazoezi ya viungo. Siku moja walikuwa mahali hadi ikafika usiku sana, lakini marehemu alitaka awahi Gym afanye angalau mazoezi nusu saa kabla ya kuelekea nyumbani. Wengi hatukujua alikuwa mpenda mazoezi.
 
Ibada iliendelea kwa nyimbo, sala na wahudhuriaji kutoa heshima zetu za mwisho mbele ya jeneza, kabla ya kusafirishwa Dar es Salaam, leo Jumatatu.
 
Idhaa ya BBC Swahili ambayo ilihusika sana na matayarisho haya ikisaidiana na Israel Saria, mwanahabari wa michezo anayeendesha tovuti ya Tanzania Sports, iliwakilishwa na watangazaji wengi maarufu wakiwemo pia Charles Hillary, Idi Sefu, Zuhura Yunus na Peter Musembi.

Akitoa neno lake Israel Saria alisema alijuana na Freddy Mtoi toka Tanzania. Saria ataisindikiza maiti  inayotarajiwa kuwasili Dar es Salaam Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, kwa ndege ya British Airways, Jumanne saa moja asubuhi. 
 
Mipango ya Ibada na mazishi Tanzania itafanyika nyumbani kwa wazazi wake Tabata Maduka Manne jijini Dar es Salaam, saa Saba mchana Jumatano. 
Mazishi yatafanyika makaburi ya Kinondoni , Jumatano hiyo hiyo saa tisa alasiri.

Habari zaidi  tembelea:

No comments:

Post a Comment