Thursday 6 December 2012

NYUKI WALETA KIZAAZAA MSIBANI MOSHI, NI BAADA YA USIA WA MAREHEMU KUPUUZWA


Ø Nyuki waleta kizazaa msibani
Ø Ni baada ya usia wa marehemu kupuuzwa.

NA SEIF MANGWANGI, MOSHI
MWENYEKITI wa Halmashauri wa Wilaya ya Moshi Vijijini, Morris Makoyi juzi alilazimika kuongoza mamia ya waombolezaji kutimua mbio kuokoa roho zao baada ya kushambuliwa na kundi la nyuki waliovamia msiban.

 Tukio hilo la aina yake, na lisilo la kawaida lilitokea baada ya kuzikwa kwa marehemu Agnes Malya(30) ambaye inasemekana aliacha usia kuwa kusiwe na mbwembwe kama vile  vyakula, pombe,  suti na sare zingine  katika mazishi yake.

Katika mbio hizo za kuokoa maisha baada ya kundi kubwa la nyuki kuvamia mwishoni mwa msiba huo, Makoyi akiongozana na Paroko wa Parokia ya Mkombole aliyefahamika kwa jina moja la Ephraim waliacha magari ya kifahari waliyofika nayo msibani na kukimbilia mgombani.

Nyuki hao wakiwa katika makundi makubwa matano walijitokeza na kuanza kuwashambulia waombolezaji hao mara baada ya mazishi ya marehemu Agnes Malya (30) aliyezikwa katika Kijiji cha Osaki Wilaya ya Moshi vijijini.

Tukio hilo ambalo si la kawaida linahusishwa na madai ya kupuuzwa kwa usia wa marehemu ambaye alipinga kuandaliwa kwa vyakula na vinywaji vitu ambavyo vitagharimu fedha ambazo zingetosha kugharamia matibabu yake kutokana ugonjwa wa kansa ya ziwa uliogharimu maisha yake .

Kutokana na kizaazaa hicho chakula na vinywaji vyenye  thamani ya zaidi ya  shilingi milioni tano vinasemekana vilimwagwa kama ishara ya kutimiza alichokisema marehemu Agnes . Lakini hilo lilifanyika baada ya nyuki kuwakumbusha waombolezaji juu ya usia wa marehemu.

Kutokana na tukio hilo,baadhi ya waombolezaji walikimbizwa katika vituo vya afya vilivyo karibu na kijiji hicho akiwamo wifi  wa marehemu  ambaye inasemekana ndiye aliyeandaa chakula katika msiba huo.

Wifi huyo, Mary Sambeke aliumwa na nyuki mwili mzima na kulazimika kuvua nguo zote hadharani na baadaye alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC ambako aliongezewa maji ya dawa(drip) ili kuokoa maisha yake.

Majeruhi wengine nane walilazwa katika Hospitali ya Misheni ya Kibosho ambako walipatiwa huduma ya kwanza na kisha kuruhusiwa kurudi nyumbani.

“Marehemu aliacha usia kutokana na ndugu wa marehemu mumewe kukataa kuchangia matibabu yake wakati akiwa hospitali , basi wasije wakajidai kuandaa sherehe wakati akifa kwa kupika vyakula na vinywaji si mnaona shughuli ya kumzika imekwenda vizuri ila kabla watu hawajala ndio nyuki wakajitokeza ?
”alisema mmoja wa ndugu wa marehemu ambaye hakutaka jina lake litaandikwe gazetini

Kwa upande wake Mwenyekiti wa halmashauri ya Moshi Vijijini ambaye pia ni diwani wa kata ya Ukaoni, Morris  Makoyi akizungumzia tukio hilo alisema ni mara ya kwanza kuona tukio la namna hiyo na limemshtua mno.

“Tulilazimika kukimbia mbio kuokoa maisha yetu,ni tukio la kushangaza sana nyuki wengi kiasi kile kutokea kusikojulikana na kuanza kushambulia waombolezaji kabla ya kumaliza shughuli za mazishi”

“Kuna tetesi na madai kuwa marehemu hakutaka chakula wala vinywaji wakati wa mazishi yake vitu ambavyo gharama  zake zingetosha kumtibu ugonjwa uliomwua sasa sina hakika kama ni kweli,”alisema Mwenyekiti huyo anayedaiwa kutaka kumng’oa Dk Cyril Chami katika nafasi ya ubunge katika uchaguzi mkuu ujao jimbo la Moshi Vijijini. 

Kaka wa marehemu aliyefahamika kwa jina la Peter Mwacha inasemekana alilazimika kuwa dereva wa bandarini kutokana na kuyasogeza magari ya waombolezaji  zaidi ya 50  kwa umbali wa mita kadhaa kutoka msibani kutokana na wenye magari hao kutawanyika ovyo kukimbia nyuki hao

Mmoja wa waombolezaji aliyejitambulisha kwa jina la Temba aliwalaumu ndugu wa marehemu kwa kukiuka usia marehemu ambaye aliweka bayana kwamba asingependa sherehe na madoido ya aina yoyote katika msiba wake.

 “Kabla na wakati wa mazishi nilikuwa nikikumbusha alichosema marehemu lakini hawakutaka kusikia sasa matokeo yake ndio haya, “alisisitiza Temba

Wakizungumzia tukio hilo baadhi ya waombolezaji walishauri jamii kubadili mtizamo wake kwa kuchangia mambo ya msingi kama kuwachangia wagonjwa katika matibabu badala ya kutoa michango mikubwa pindi mgonjwa anapofariki.

“Lazima tubadilike badala ya kuchanga mamilioni kwenye mazishi tuchange kumnusuru mgonjwa ili yeye mwenyewe atambue mchango ule badala ya kuchangia maiti”alisema mmoja wa waombolezaji ambaye hakupenda jina lake litajwe gazetini.

Tofauti na wengine,Watanzania wamekuwa wepesi kutoa michango mikubwa katika shughuli za sherehe na misiba badala ya kuwachangia wagonjwa na wanafunzi wa shule au  vyuo kama wanavyofanya Kenya na Uganda na nchi zingine.

ends
  

No comments:

Post a Comment